 |
| Wakaazi wakisaidiana na mfanyikazi wa Red Cross kumhudumia mhasiriwa |
Hofu na huzuni zimetanda katika maeneo ya Gamba, Kaunti ya Tana river na Hindi, Kaunti ya Lamu baada ya zaidi ya watu 30 kuuwawa kwa kupigwa risasi kwenye Mashambulizi mawili yaliyotekelezwa usiku wa kuamkia leo.
Kulingana na kamanda wa polisi katika kanda ya Pwani, Robert Kitur, watu 9 akiwemo afisa mmoja wa polisi wameuwawa huku mtu mmoja akijeruhiwa vibaya katika eneo la Gamba, mji wa Garseni baada ya watu waliojihami kwa risasi kukivamia kituo cha polisi cha Gamba na kumtorosha mshukiwa mmoja wa mauaji ya mpeketoni aliyekuwa anazuiliwa kwenye kituo hicho.
Wakati huo huo watu saba wameuwawa katika eneo la Hindi,lililoko kilomita chache kutoka mji wa Mpeketoni ambapo zaidi ya watu 60 waliuwawa katika hali ya kutatanisha majuma kadhaa yaliyopita.
Kwenye tukio la Hindi, nyumba kadhaa na magari ya meteketezwa huku watu watano walio na majeraha mabaya ya risasi wakiendelea kuuguza majeraha katika hospitali ya King Fahad, kaunti ya Lamu.
Kituo cha kitaifa cha kukabiliana na majanga, NDOC kimesimulia kupitia ukurasa wake wa twitter kuwa makabiliano makali ya risasi yalizuka katika eneo la kibiashara la Hindi karibu na Mpeketoni, usiku wa kuamkia leo.
Maafisa wa polisi wakishirikiana na shirika la red cross wanaendelea na operesheni ya kuwaokoa wahasiriwa huku wakiwasaka wavamizi hao.
Hata hivyo kiini cha mauaji hayo hakijabainika huku msemaji wa kundi la wanamgambo wa Al shabab, Abdulazizi Abu Musab akikiri kuwa kundi hilo limetekeleza ukatili huo jambo ambalo Rais Uhuru Kenyatta amelpinga vikali na kuhoji kuwa mauji hayo yamechochewa kisiasa.
Uvamizi huu unajiri licha ya serikali kuwahakikishia raia usalama wao huku mrengo wa upinzani wa Cord ukitarajiwa kuandaa mkutano wake wa Sabasaba katika bustani la Uhuru, jijini Nairobi, hapo kesho.