Viongozi wa baraza kuu la Waislamu nchini Kenya, (Supkem)
kutoka kaunti ya Garissa wametoa wito kwa serikali itekeleze mabadiliko kwa
wasimamizi wa uslama mjini Mombasa kwa kutowajibika.
Wakizungumza mjini Garissa mapema leo, viongozi hao
wakiongozi na Mwenyekiti wa Supkem mjini humo, Abdullahi Salat, wamewalaumu
maafisa wakuu wa uslama mjini Mombasa kwa ongezeko la visa vya utovu wa usalama.
"Tunamuomba Rais Uhuru Kenyatta, awafanyie mabadiliko
Wakuu wa usalama mjini Mombasa, kwa sababu wengi wao wamekuwa na ukatili dhidi
ya wenyeji wanaostahili kuwalinda na hivyo basi kusababisha kutoaminiana",
Abdullahi amesema.
Aidha viongozi hao wamelaani vikali hatua ya kufungwa kwa
misikiti na kufurushwa kwa waumini mara kwa mara huku wakidai kuwa huenda hali hiyo ikaathiri uwiano mjini humo. Badala yake, viongozi hao wameiri serikali
kutumia mbinu mbadala za kupambana na washukiwa wa uhalifu bila kuwalenga
waumini.
Vilevile, Abdullahi amewaonya maafisa wa usalama dhidi ya
kulenga misikiti huku akieleza kuwa misikiti ni eneo muhimu la ibada wala sio
maskani ya wahalifu.
Viongozi hao wa Supkem wameongeza kuwa viongoi wa kidini
ndio wanaostahili kulifumbua tatizo linalosibu mjini Mombasa kwa njia ya
mazungumzo wala sio kupitia maafisa wa usalama.
Haya yanajiri baada ya maafisa kutoka vikosi mbalimbali vya
usalama kuvamia misikiti ya Musa, Sakina na Swafaa na kuwakamata zaidi ya
vijana 200.
Kwa sasa, Misikiti hiyo iko chini ya ulinzi mkali huku
wenyeji wakilazimika kusaka njia mbadala za kutekeleza Ibada.











