Habari za kuaminika kutoka maeneo ya pwani na kaskazini mashariki mwa Kenya

Friday, 21 November 2014

SUPKEM YATAKA WASIMAMIZI WA USALAMA MOMBASA WAONDOLEWE

Viongozi wa baraza kuu la Waislamu nchini Kenya, (Supkem) kutoka kaunti ya Garissa wametoa wito kwa serikali itekeleze mabadiliko kwa wasimamizi wa uslama mjini Mombasa kwa kutowajibika.

Wakizungumza mjini Garissa mapema leo, viongozi hao wakiongozi na Mwenyekiti wa Supkem mjini humo, Abdullahi Salat, wamewalaumu maafisa wakuu wa uslama mjini Mombasa kwa ongezeko la visa vya utovu wa usalama.

"Tunamuomba Rais Uhuru Kenyatta, awafanyie mabadiliko Wakuu wa usalama mjini Mombasa, kwa sababu wengi wao wamekuwa na ukatili dhidi ya wenyeji wanaostahili kuwalinda na hivyo basi kusababisha kutoaminiana", Abdullahi amesema.

Aidha viongozi hao wamelaani vikali hatua ya kufungwa kwa misikiti na kufurushwa kwa waumini mara kwa mara huku wakidai kuwa huenda hali hiyo ikaathiri uwiano mjini humo. Badala yake, viongozi hao wameiri serikali kutumia mbinu mbadala za kupambana na washukiwa wa uhalifu bila kuwalenga waumini.

Vilevile, Abdullahi amewaonya maafisa wa usalama dhidi ya kulenga misikiti huku akieleza kuwa misikiti ni eneo muhimu la ibada wala sio maskani ya wahalifu.

Viongozi hao wa Supkem wameongeza kuwa viongoi wa kidini ndio wanaostahili kulifumbua tatizo linalosibu mjini Mombasa kwa njia ya mazungumzo wala sio kupitia maafisa wa usalama.

Haya yanajiri baada ya maafisa kutoka vikosi mbalimbali vya usalama kuvamia misikiti ya Musa, Sakina na Swafaa na kuwakamata zaidi ya vijana 200.


Kwa sasa, Misikiti hiyo iko chini ya ulinzi mkali huku wenyeji wakilazimika kusaka njia mbadala za kutekeleza Ibada.

Friday, 5 September 2014

Mombasa county unites with Constituencies for development projects

Mombasa county governor Hassan Ali Joho led various leaders from the area including Mps and Mcas on a four day development tour of Kisauni constituency a few days after a similar operation in Jomvu and Changamwe constituencies.

Speaking after commissioning of 2 solar powered boreholes in Mjambere and Magogoni wards which are expected to serve over 5000 people, Joho said the effort was aimed at combining the County’s development agenda with the development plans of various constituencies to improve the living condition Mombasa residents.

“Team work is paramount. I am glad that all levels of leadership in Mombasa County are working together as one compact unit. This is the seed that we planted almost a year ago and now the fruits are clearly visible for our people to benefit from", he said.
The governor also added that the move played a significant role in eliminating duplications and ensuring standardization in all development projects throughout the County.
 
Amongst area leaders who accompanied the  Governor, included Senator Hassan Omar, area Kisauni Mp, Rashid Bedzimba, Jomvu Mp, Badi Twalib.

The team also commissioned the Msikitini Cabro road of 350 meters at the cost of about Kshs 4.5M. 

The governor praised Kisauni Mp Bedzimba for for exhibiting efficiency and transparency in the execution of the project.
 
Joho is expected to lead the commissioning of more projects in Mwakirunge ward on Friday and Junda ward on Saturday.

Thursday, 31 July 2014

Mkufunzi wa Bandari, Twahir Muhiddin alazwa hospitalini

Kocha wa Bandari, Twahir Muhiddin
Kocha Twahir Muhiddin anayewafunza wawakilishi wa pwani katika ligi kuu ya soka humu nchini, Bandari, anaendelea kupokea matibabu katika hospitali moja mjini Mombasa baada ya kuugua.

Akithibitisha taarifa hiyo, meneja wa bandari, Charles Obwaka ameeleza kuwa Twahir amelazwa hospitalini siku ya jumamosi baada ya kupatwa na maumivu.

Obwaka ameongeza kuwa wanamatumaini kuwa Twahir atarejea katika hali ya kawaida na kuendelea kuinoa timu hiyo inayoshikilia nafasi ya kumi na moja kwenye jedwali la ligi kuu ya soka humu nchini.

Kutokuwepo kwa Twahir haikuathiri timu hiyo kwani Bandari ilijitahidi na kuondoka na sare ya goli moja dhidi ya Tusker kwenye mchuano wa ligi ulioandaliwa katika uwanja wa Mombasa siku ya jumapili.

Kufikia sasa manaibu wakufunzi wa Bandari, Ali Breik na Nassoro Mwakoba wanaendelea kuifunza timu hiyo kwa minajili ya mchuano wake wa ligi ugenini dhidi ya Mathare itakayochezwa tarehe sita mwezi ujao.

Gavana Joho amtimua waziri wa fedha, Walid Khalid

Aliyekuwa waziri wa fedha, kaunti ya Mombasa, Walid Khalid
Baada ya vuta nikuvute kati ya bunge la kaunti ya Mombasa na waziri wa Fedha, Walid Khalid, hatimaye Gavana wa Mombasa Hassan Ali Joho amemuachisha kazi waziri wake wa fedha, Walid Khalid.

Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, Joho amekariri kuwa amechukua hatua hiyo baada ya misururu ya Khalid kukumba na madai ya ukiukaji wa sheria za utoaji zabuni na ununuzi wa mahitaji ya serikali ya  kauti ya Mombasa.

Awali wabunge wa kaunti ya Mombasa waliwasilisha hoja ya kutokuwa imani na Khalid huku wakidai kuwa hawajapendezwa na utendakazi wake.

Kwa sasa Gavana Joho amemteua waziri wa vijana na michezo, Hazel Koitaba kuwa kaimu waziri wa fedha huku gavana huyo akisubiriwa kumteuwa waziri mpya wa fedha.



Uanzilishi wa taa za trafiki Mombasa, zapongezwa

Taa za trafiki zikimulika barabarani

Wamiliki wa magari ya uchukuzi mjini Mombasa wameipongea serikali ya kaunti ya Mombasa kwa kufanikisha taa za trafiki.

Wakiongozwa na mfanyibiashara maalum,na mmiliki wa kampuni moja ya mabasi, Mohamed Ibrahim, wafanyibiashra hao wameeleza kuwa taa hizo zimepunguza ajali za barabara pamoja na msongamano wa magari mjini Mombasa.

Kwa upande wake waziri wa uchukuzi mjini Mombasa, Mohamed Abbass, ametoa ufafanuzi kuwa serikali ya kaunti hiyo imechukua hatua hiyo kama njia moja ya kuimarisha sekta ya uchukuzi mjini humo.

Abbass ameongeza kuwa serikali hiyo inalenga kuzidisha idadi ya taa hizo katika maeneo mengine mjini humo ili kuzuia msongamano wa magari na ukiukaji wa sheria za barabarani.

Taa hizio zimewekwa katika barabara mbalimbali kama vile, Buxton, Digo na Sabasaba.





Viongozi wa Mombasa wataka miraa ipigwe marufuku

Zao la miraa linalotaka kupigwa marufuku
Viongozi mbalimbali mjini Mombasa, wameapa kuhakikisha kuwa zao la miraa limepigwa marufuku mjini humo huku wakiilaumu kwa uzembe na kudorora kwa afya ya wakazi wa mji huo.

Wakiongozwa na mbunge wa Changamwe, Omar Mwinyi na mwenzake wa Jomvu, Badi Twalib, na wabunge mbalimbali wa kaunti, viongozi hao wamemrai gavana wa mombasa, Hassan Ali Joho, apige marufuku uuzaji na utumizi wa miraa huku viongozi hao wakidai kuwa idadi kubwa ya wenyeji wa kaunti hiyo wameathirika pakubwa na matumizi ya zao hilo huku mamilioni ya fedha zikitumika kwa ununuzi wake.

Kwa upande wao wabunge wa kaunti wametoa wito kwa wabunge wenzao waunge mkono mpango huo huku wakihoji kuwa hatua hiyo itakuw ana manufaa makubwa kwa maendeleo ya kaunti hiyo.

Kauli ya viongozi hawa inajiri wiki chache tu baada ya bunge la kaunti ya Mombasa kupinga mswada dhid ya miraa uliowasilishwa na mwakilishi wa wodi mteule, Fatma Swaleh.

Madereva wengi mjini Mombasa wamelaumiwa kwa kuendesha magari wakitumia miraa huku wakihatarisha maisha ya maabiria.

Hata hivyo mamlaka ya kitaifa ya kudhibiti vileo na mihadarati, Nacada, imeambia serikali ya kaunti ya mombasa iuende sheria itakayoongoza juu ya uuzaji na utumiaji wa miraa katika maeneo muhimu mjini humo.

Mtalii wa Kijerumani auwawa Mombasa

Watalii wakiwasili humu nchini
Taharuki imetanda mjini Mombasa baada ya mtalii mmoja kutoka Ujerumani kuuwawa kwa kupiga risasi katika mtaa wa Mji wa Kale, mjini Mombasa usiku wa kuamkia leo.

Mtalii huyo, ChristineTex mwenye umri wa miaka 30, alifariki papo hapo baada ya watu waliojihami kwa bnduki kuwamiminia risasi yeye pamoja na mchumba wake, Henri Sekandi.

Kulinga na mkuu wa idara ya polisi wa utalii, mjini Mombasa,Robert Sicharani, mwanamke huyo alikuwa pamoja na mchumba wake kutoka Uganda huku wawili hao wakiwa katika ziara ya kitalii katika mji wa kihistoria wa Mji wa kale.

Kwa upande wake, Khalid Ibrahim, ambaye ni msimamizi wa polisi jamii katika mtaa wa mji wa kale, ameeleza kuwa mwanamke huyo aliuwawa bila kuibiwa chochote huku kiini cha mauaji yake kikisalia kuwa kitendawili.

Mji wa Kale umekuwa ukishuhudia mauaji ya watalii ya mara kwa mara kwani miezi michache iliyopita, watalii watatu kutoka urusi walishambuliwa na kuuwawa kwa kupigwa risasi.

Polisi wanaendeleza uchunguzi ili kubaini chanzo cha mauaji hayo.

Sunday, 6 July 2014

Zaidi ya watu 30 wauwawa katika kaunti za Lamu na Tana River

Wakaazi wakisaidiana na mfanyikazi wa Red Cross kumhudumia mhasiriwa















Hofu na huzuni zimetanda katika maeneo ya Gamba, Kaunti ya Tana river na Hindi, Kaunti ya Lamu baada ya zaidi ya watu 30 kuuwawa kwa kupigwa risasi kwenye Mashambulizi mawili yaliyotekelezwa usiku wa kuamkia leo.

Kulingana na kamanda wa polisi katika kanda ya Pwani, Robert Kitur, watu 9 akiwemo afisa mmoja wa polisi wameuwawa huku mtu mmoja akijeruhiwa vibaya katika eneo la Gamba, mji wa Garseni baada ya watu waliojihami kwa risasi kukivamia kituo cha polisi cha Gamba  na kumtorosha mshukiwa mmoja wa mauaji ya mpeketoni aliyekuwa anazuiliwa kwenye kituo hicho.

Wakati huo huo watu saba wameuwawa katika eneo la Hindi,lililoko kilomita chache kutoka mji wa Mpeketoni ambapo zaidi ya watu 60 waliuwawa katika hali ya kutatanisha majuma kadhaa yaliyopita.

Kwenye tukio la Hindi, nyumba kadhaa na magari ya meteketezwa huku watu watano walio na majeraha mabaya ya risasi wakiendelea kuuguza majeraha katika hospitali ya King Fahad, kaunti ya Lamu.

Kituo cha kitaifa cha kukabiliana na majanga, NDOC kimesimulia kupitia ukurasa wake wa twitter kuwa makabiliano makali ya risasi yalizuka katika eneo la kibiashara la Hindi karibu na Mpeketoni, usiku wa kuamkia leo.

Maafisa wa polisi wakishirikiana na shirika la red cross wanaendelea na operesheni ya kuwaokoa wahasiriwa huku wakiwasaka wavamizi hao.

Hata hivyo kiini cha mauaji hayo hakijabainika huku msemaji wa kundi la wanamgambo wa Al shabab, Abdulazizi Abu Musab akikiri kuwa kundi hilo limetekeleza ukatili huo jambo ambalo Rais Uhuru Kenyatta amelpinga vikali na kuhoji kuwa mauji hayo yamechochewa kisiasa.

Uvamizi huu unajiri licha ya serikali kuwahakikishia raia usalama wao huku mrengo wa upinzani wa Cord ukitarajiwa kuandaa mkutano wake wa Sabasaba katika bustani la Uhuru, jijini Nairobi, hapo kesho. 

Thursday, 3 July 2014

Mwezi wa Ramadhan yawanufaisha wanabiashara Mombasa

Muuzaji akiwa na mteja kwenye kibanda cha kuuza vyakula

















Wafanyibiashara wa Mombasa wanaendelea kufurahia mapato ya uuzaji wa bidhaa mbalimbali kwenye mwezi wa ramadhan huku waumini wa kiislamu wakitekeleza ibada ya saum.

Wafanyibiashara wa soko la Markiti, mwembe tayari na soko kuu la kongowea wameshuhudia ongezeko la wateja huku biashara zao zikipigwa jeki na hatua ya serikali ya kaunti ya Mombasa ya kuondoa marufuku kwa wachuuzi wa vyakula katika maeneo ya kibiashara mjini humo.

Wengi wa Wafanyibiashara wanaoendelea kunufaika ni wauzaji wa vyakula na vifaa vya nyumbani huku ongezeko la bei za bidhaa hizo likishuhudiwa kutokana na maandalizi ya mlo wa kufungua saumu jioni wa iftar na mlo wa mwisho wa usiku wa daku na waumini wa kiislamu.

Tende, madafu, unga, matunda, mboga na nyama ni baadhi ya bidhaa zenye mvuto mkubwa kwa wateja hao kutokana na umuhimu wa bidhaa hizo katika mwezi wa Ramadhan.

Waumini hao wa kiislamu hutekeleza ibada ya saum ya siku 29 au 30 kila mwezi wa tisa katika kalenda ya kiislamu.


Thursday, 26 June 2014

Hatujarudisha hata senti kwa serikali kuu,asema Gavana wa Garissa, Nathif Jama

Ismail Haki, kutoka shirika la TIKA (kulia) na Gavana wa Garissa, Narthif Jama.















Gavana wa Kaunti ya Garissa, Nathif Jama, amepuuzilia mbali madai kuwa serikali yake imerudisha bilioni moja nukta mbili ya pesa iliyotengewa na serikali kuu kwa minajili ya maendeleo ya kaunti hiyo.
 
Akiwahutubia wananchi katika mji wa Garissa baada ya kupokea magari ya kuokota taka yaliyotolewa na shirika la kituruki la TIKA, Jama alijitetea na kusema kuwa waliutumia mgao wao vyema "Kaunti yetu haiwezi ikachukua hatua kama hiyo . Tumezitumia fedha tulizotengewa kufadhili miradi mbalimbali katika kaunti hii", alisema.

Nathif ametofautiana na ripoti hiyo iliyowasilishwa kwa bunge la seneti na msimamizi wa bajeti huku akihoji kuwa serikali yake imeshuhudia upungufu wa fedha kinyume cha madai kuwa haikuweza kutumia fedha ilizotengewa vikamilifu.

Wakati huo huo, Gavana huyo ameishukuru serikali ya uturuki kwa msaada huo huku akiwataka wenyeji wa mji huo kuyatumia magari hayo vyema ili kufanikisha usafi katika mji huo.

Kwa upande wake, Mwakilishi wa serikali ya Uturuki, Ismail Haki, ameahidi kuwa serikali hiyo itaendelea kuunga mkono miradi ya maendeleo katika kaunti hiyo na serikali ya Kenya.

"Tutaendelea kufanya kazi na wenyeji wa kaunti ya Garissa ili kuboresha maisha yao. Tulikuwa pamoja wakati wa kiangazi na tutazidi kushirikiana nanyi," alimaliza bwana Ismail.

Msaada huo wa magari umepiga jeki hatua za kuleta usafi katika mji huo huku wenyeji wakijawa na matumaini kuwa magari hayo yatatumika vyema.

Arsenal yawatimua wachezaji kumi na moja


Miamba wa soka nchini uingereza na mabingwa wa Kombe la F.A, Arsenal fc imetangaza rasmi kuwa imetengana na wachezaji kumi na moja wa timu hiyo ili kutoa nafasi kwa wachezaji wanaotaka kuwasajili.

Kupitia taarifa kwenye mtandao wake wa Arsenal.com, mshambulizi matata wa Denmark, Niklas Bendtner na nahodha wa zamani wa Korea kusini J.Y Park wameihama timu hiyo baada ya mkataba wao kumalizika.

Wakati huo huo, wachezaji waliojiunga na timu hiyo kwa njia ya mkopo, Kim Kallstrom wa Sweden na kipa Emiliano Viviano watarejea kwa wamiliki wao baada ya kutumikia mda wao wa mkopo ugani emirates.

Aidha mdakaji Lukasz Fabianski, beki Bacary Sagna na kiungo Zak Ansah wameihama timu hiyo baada ya kudinda kurefusha kandarasi zao an timu hiyo.

Wengine walioigura timu hiyo ni wachezaji chipukizi, Chuks Aneke na Daniel Boateng, Zach Fagan na Leander Siemann.

Kutoka hapa mtitigo, tunawatakia mastaa hao kila la heri popote watakapokwenda kusakata kambumbu.





Chuo kikuu cha Technical University of Mombasa chafungwa






















Shughuli za masomo zimekatizwa katika tawi kuu la chuo kikuu cha kiufundi cha Mombasa  kufuatia mgomo wa wanafunzi wa chuo hicho.

Wanafunzi wa kozi za uhandisi wanadaiwa kuanzisha mgomo huo huku wakidai kuwa chuo hicho hakina uwezo wa kutoa kozi hiyo na badala yake sasa wanataka wahitimu kozi hiyo katika chuo kikuu cha kilimo na teknolojia Jomo kenyatta.

Hata hivyo wanafunzi hao hawajasababisha uharibifo wowote licha ya maafisa wa polisi kuingilia kati na kuufurusha mgomo huo kwa kutumia vitoa machozi.

Kwa sasa wasimamizi wa chuo hicho wanaendelea na mazungumzo kwenye mkutano wa dharura ili kulifumbua tatizo hilo.

Wanafunzi wote wa chuo hicho wamepewa ilani ya kuondoka haraka iwezekananvyo hadi pale watakapofahamishwa tarehe mpya ya kufunguliwa kwa chuo hicho.


Wednesday, 25 June 2014

Gavana wa Lamu, Issa Timamy matatani kwa mauaji ya Mpeketoni

Gavana wa Kaunti ya Lamu, Issa Timamy.
Gavana wa kaunti ya Lamu Issa Timamy anatarajiwa kufikishwa mahakamani hii leo kufuatia mauaji ya hivi majuzi ya zaidi ya watu 60 katika eneo la Mpeketoni, kaunti ya Lamu.

Gavana Timamy alikamatwa mjini Mombasa siku ya Jumatano na maafisa wa idara ya upelelezi ya CID na kuzuiliwa katika afisi za idara hiyo kwa saa kadhaa ili kuhojiwa.

Kaunti ya Lamu imekuwa chini ya kurunzi kali ya serikali kufuatia mashambulizi ya mara kwa mara yaliyotekelezwa na watu wasiojulikana na kuwa tishio kubwa kwa usalama wa wenyeji wa kaunti hiyo.

Hata hivyo chanzo cha mauaji katika kaunti hiyo hakijabainika kufikia sasa licha ya Rais Uhuru Kenyatta kueleza kuwa uvamizi katika eneo la mpeketoni lilichochewa kisiasa.

Kundi la wanamgambo la Al Shabaab lilijitokeza na kukiri kuwa lilitekeleza shambulizi la eneo la Mpeketoni huku kundi hilo likiitaka serikali iwaondoe wanajeshi wake walioko nchini Somalia.

Timamy aliponea na kusalia kuwa gavana mnamo mwezi Novemba mwaka uliopita baada ya mahakama ya rufaa kufutilia mbali uchaguzi mdogo wa ugavana ulioratibiwa kufanywa na tume huru ya uchaguzi na mipaka, IEBC.

Monday, 23 June 2014

Watu 30 wauwawa katika kaunti za Wajir na Mandera



Viongozi wa Kaunti za Wajir na Mandera wakiwa katika eneo la Wajir

















Huzuni imetanda katika kaunti za Wajir na Mandera baada ya watu 30 kufariki kufuatia mapigano mapya kati ya jamii za Garre na Degodia.

Akithibitisha mauaji hayo, Msemaji wa polisi Gatiria Mboroki amesema kuwa watu wa koo ya Gegodia wanadai wizi wa mifugo yao na mahasimu wao kutoka jamii ya Gare na kupelekea vita hivyo katika eneo la Gunan.

Wakati huo huo, familia 35 zimeachwa bila makao baada ya nyumba zao kuteketezwa kwenye mapigano hayo huku watu watano wakijeruhiwa vibaya.

Maafisa kutoka kitengo cha GSU, polisi wa kawaida na KDF wa kambi ya Elwak wametumwa eneo hilo kudhibiti hali huku kukiwa na ripoti kwamba watu wengine watano walijeruhiwa vibaya kwenye ghasia hizo na nyumba 35 kuteketezwa.

Kiongozi wa waliowengi bungeni, Aden Dualle amelaani vikali mauaji hayo huku akiongeza kuwa jamii hizo zinastahili kukumbatiua amani ili kuzuia umwagikaji wa damu.

Mradi wa ujenzi wa barabara ulioanzishwa na serikali ya kaunti ya Wajir umelaumiwa kwa mapigano hayo huku jamii hizo zikiendelea kuzozania mpaka kati ya kaunti hizo.
Hatua za viongozi wa kisiasa na wa kidini kuzipatanisha koo hizo mbili zimegonga mwamba huku hali ya taharuki ikitanda kati ya watu wa jamii hizo mbili.

Kwa sasa wenyeji wa kaunti hizo wanaitaka serikali iwakamate viongozi wa kisiasa kwa uchochezi  huku watu 40 wakiwa wamefariki na wengine wafikao 100 wakiachwa bila makao ndani ya kipindi cha  mwezi moja tu kwenye ghasia hizo.